SOMA
NENO, TAFAKARI NENO, TENDA NENO
By
CLEMENT EMMANUEL a.k.a RICH IN JESUS
Mobile
no:
0717740706 & 0752570017
E-mail:
rijmanu@gmail.com & emmanuelc15@yahoo.com
blog : yotekwayesu.blogspot.com
SALAMU ZA AWALI KABLA
YA SOMO
BWANA Yesu apewe sifa
sana ndugu mpendwa! mimi binafsi najisikia furaha sana kiasi kwamba nashindwa hata
kuelezea. Nina furaha kubwa kwa sababu bwana Yesu ameamua yeye mwenyewe
kukufikia wewe ndugu msomaji kupitia somo hili, ambalo alianza kunifundisha
mimi kwanza kwa uwezo wa Roho wake Mtakatifu, kisha akanipa kibali niweze
kukufikia pia wewe ndugu yangu msomaji, ili sote tupate kuzingatia maagizo yake
kisha tuweze kupata mafanikio hapa dunia kisha kuingia katika uzima wa milele.
Mimi binafsi
ninamrudishia sifa Mungu kupitia mwanawe mpendwa Yesu kristo BWANA na mwokozi
wa maisha yangu. Kwani ndiye aliyekiandika kitabu hiki yeye mwenyewe kupitia uwezo
wa Roho Mtakatifu wake akaaye ndani yangu. Roho Mtakatifu msaidizi wangu mwema,
Amekuwa mwaminifu mno akinielekeza mimi kama chombo tu ni kitu gani niandike
ili makusudi ya Mungu yatimizwe juu yako wewe ndugu msomaji.
Ninajua ya kwamba
shetani hapendi kabisa wewe unayesoma kitabu hiki upate ufahamu juu ya maneno
ya Mungu, tena hapendi kabisa upate kuelewa mawazo mema ya Mungu juu ya maisha
yako. Kwani anajua mafanikio ya maisha yako yanatoka kwa Mungu pekee, pia siri
zote za maisha zipo kwenye NENO la Mungu pekee. Sasa ninajua shetani ambaye ni
baba wa uongo na jeshi lake wamejipanga vizuri sana kukuzuia usiweze kujua siri
za ufalme wa mbinguni kupitia kitabu hiki. Lakini
kwa jina la Yesu kristo lipitalo majina yote (wafilipi 2:9-11), ninakuamuru shetani umwache ndugu msomaji
anayetaka kusoma siri hizi na ukimbilie kuzimu ukateketee huko kwa mamlaka ya
jina laYesu kristo, kwani imeandikwa katika (ufunuo 12:11) ya kwamba “Nao wakamshinda kwa damu ya
mwana-kondoo,.…..”, nami sasa kwa damu ya Yesu kristo ninazitakasa fahamu za
ndugu msomaji na ninakuamuru wewe shetani katika jina lipitalo kila jina, jina
la Yesu kristo! uziache kabisa fahamu za ndugu msomaji, ili msomaji apate
kuelewa siri ambazo Mungu ameziweka leo mbele yake kupitia kitabu hiki.
Ndugu msomaji katika
jina la Yesu! Ninakukaribisha sasa ili tuweze kutafakari kwa pamoja maneno ya
Mungu, ila nakusihi usome kwa kutafakari na ninakuhakikishia ya kwamba msaidizi
wetu Roho Mtakatifu yupo nawe hivi sasa, ili kukusaidia wewe ndugu msomaji
uweze kuelewa na kuyatendea kazi maneno ya Mungu utakayosoma katika kitabu hiki.
HEBU
SASA NA TUANZE SOMO LETU KWA PAMOJA, KATIKA JINA LA YESU!
NDUGU
YANGU MPENDWA KATIKA JINA LA YESU KRISTO WA NAZARETI ALIYE HAI, NAOMBA TUANZE SOMO LETU KWA KUJIULIZA MASWALI
YAFUATAYO ;-
Ø NENO
NI NINI?
Ø KWA
NINI TUSOME NENO?
Ø JE
NI KWELI TUKISOMA NENO, TUNAMSOMA YESU?
Ø NINI
HASARA YA KUTOSOMA, KUTOTAFAKARI NA KUTOTENDA NENO?
Ø NINI
FAIDA YA KUSOMA, KUTAFAKARI NA KUTENDA NENO?
Ø KIPI
BORA! FAIDA AU HASARA?
NENO
NI NINI ?
Neno ni mkusanyiko wa herufi ambazo zikiunganishwa
zinetengeneza maandishi ambayo yanaleta maana kwa msikilizaji au msomaji wa
maandishi hayo, au tafsiri nyingine ya neno inasema, Neno ni mazungumzo
yanayolenga kuelezea kitu Fulani, au wengine hutafsiri kwa kusema, Neno ni
maagizo yatolewayo kwa mtu kwa njia ya maandishi au kwa njia ya mazungumzo.
Najua unaweza ukawa na tafsiri nyingi mno za neno kwa kadiri unavyoelewa, mimi
ninajua ya kwamba upo sahihi kabisa kwa tafsiri ulizo nazo. Lakini mimi nimeona
ni vema tuzitumie hizi chache nilizoziandika katika kitabu hiki.
Mimi ningependa tuangalie tafsiri ya neno kama,
“maagizo yatolewayo kwa mtu kwa njia ya maandishi au kwa njia ya mazungumzo,
yakilingenga kuelezea kitu Fulani chenye manufaa kwa msomaji au msikilizaji,
Ili tu aweze kupata kuelewa na mara nyingine uweze kutenda kitu kilichokusudiwa
ndani ya mazungumzo hayo” kwa mfano mtu akikwambia neno imba! Mtu huyo
anatarajia kukuona ukiimba, usipoimba inamaanisha ya kwamba; pengine hujasikia
neno hilo au umeacha kutenda sawa sawa na neno hilo.
NENO LA MUNGU unaweza ukaritafsiri kama maana
nyingine za neno lakini tofauti kubwa iliyopo ni kwamba neno la Mungu li hai na
mtu akilizingatia na kulitenda linamletea usitawi na mafanikio kama linavyosema
neno la Mungu katika Joshua 1:8.
Sasa basi ni vema wewe ukatambua kwamba Mungu wetu
huwa hafanyi kitu ambacho kipo nje ya neno lake, ndio maana katika yeremia 1:12b Bwana akasema “kwa maana
NINALIANGALIA NENO LANGU, ILI NILITIMIZE ”
Kwa hiyo neno la Mungu ni la muhimu sana kwa maisha bora ya mkristo yeyote
asiyetaka kuangamia kwa kukosa maarifa, kwani hosea 4:6 inasema ya kwamba “watu wangu wanaangamizwa kwa kukosa
maarifa;……………………………………….”
KWA
NINI TUSOME NENO?
Katika hali ya kawaida ukuaji wa kiumbe chochote
hutegemea sana ni vitu gani anavyokula, sasa basi ili kiumbe hai yeyote akue
vizuri anatakiwa ale chakula kilichokamilika yaani kwa kiingereza (balanced
diet) ili apate kuwa na afya njema.
Ukitaka kuangalia ukuaji wa kiumbe hai chochote hasa binadamu angalia ni vyakula gani
anavyokula. Akiwa na afya mbaya, sisi tutajua tu kwamba chakula anachokula kina
mapungufu au labda pengine huwa anakula kwa shida sana na ndio maana
anadhoofika.
Akiwa na afya nzuri tutajua tu ya kwamba binadamu
huyu anakula chakula bora na chenye virutubisho vyote muhimu kwa afya yake.
Sasa basi kama ukuaji wa binadamu kimwili hutegemea
chakula bora. Basi pia ukuaji wa binadamu kiroho hutegemea chakula bora chenye
virutubisho vyote kiroho yaani NENO la MUNGU litokalo kwenye kinywa cha MUNGU
ambalo siku zote hutimiza mapenzi ya mungu (Isaya 55:11).
Labda nikumegee siri kidogo ndugu yangu ya kwamba “
AMINI USIAMINI MAFANIKIO YAKO YOTE YAPO KWENYE NENO LA MUNGU yaani MAANDIKO
MATAKATIFU”.
Mtu mwingine anaweza asielewe kabisa kwamba
mafanikio yake yote yapo kwenye neno la MUNGU, aah! ndugu yangu mpendwa. Mimi
binafsi nilianza kuona mafanikio mengi kwenye maisha yangu ya wokovu, baada ya
kuanza kulisoma na kulitafakari neno la MUNGU lakini kabla ya hapo nilikuwa
ninajiona nipo kawaida sana yaani nilikua na utapia mlo wa kiroho ambao ulizuia
mafanikio yangu katika Nyanja zote za kimaisha yaani kiroho na kimwili. Hehu
jiulize ni kwa nini MUNGU alimwambia Joshua mwana wa Nuni ya kwamba “kitabu
hiki cha torati kisiondoke kinywani mwako, bali YATAFAKARI maneno yake mchana
na usiku, upate kuangalia KUTENDA sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo;
ndipo UTAKAPOIFANIKISHA njia yako, kisha ndipo UTAKAPOSITAWI sana” Joshua 1:8 . sasa hebu tujiulize kwa
pamoja ni kwa nini MUNGU katika maagizo yake ya kwanza kabisa kwa Joshua aamue
kumsisitizia habari ya umuhimu wa maneno
ya torati juu ya kufanikiwa na kusitawi katika kila alilolifanya, Ni kwa nini asingembwambia
fanya maombi sana au sifu sana?. Naomba uelewe vema kabisa ya kwamba NENO LA
MUNGU linabeba kila kitu cha KIMUNGU ambacho kinapelekea mafanikio yote ya KIMUNGU
pia. Kwa sababu kama ni maombi yameandikwa kwenye neno kama ni sifa na kuabudu
vipo kwenye neno kama ni ndoa inafundishwa kupitia neno, kama ni hekima
inapatikana kupitia neno la Mungu, kwa kifupi neno ni kila kitu kwa mtu
anayetarajia kwenda mbinguni yaani MLOKOLE.
Ni wazi kabisa ya kwamba Joshua asingezingatia
torati inasema nini juu ya safari ya wana wa Israeli pengine kaanani(nchi ya
ahadi) ingekuwa ndoto kwa wana wa Israeli. Ndio sijakosea! namaanisha kaanani
ingekuwa ndoto kwa wana israeli, pengine na kwako pia ukiliacha neno la Mungu
MBINGUNI utapasikia kwenye redio tu.
Si hivyo tu ukiacha kusoma neno la MUNGU, pia
ukiacha kutafakari neno na tena ukiacha kutenda sawa sawa na neno la MUNGU,
mafanikio kwako itakuwa shida na kusitawi kwako kunaweza kukawa na matatizo
mengi na mashaka ndani yake. Ndio maana leo roho mtakatifu ameamua kukukumbusha
ya kwamba SOMA NENO,TAFAKARI NENO, TENDA NENO!
Hebu tuangalie pia Zaburi 119:105 “neno lako ni taa ya miguu yangu, na mwanga wa njia
zangu ” ukiangalia maneno hayo ya zaburi utagundua ya kwamba usipolijua neno la
MUNGU miguu yako na njia zako zitakuwa giza totoro. Sasa basi ukitaka mwaga pia
taa ikuwakie katika maisha yako yote ni vema ukachukua taa hii yaani neno kwani
taa hii haiishiwi nguvu hata siku moja.
Ukiangalia pia mithali
16:20a “Atakayelitafakari neno atapata mema;” sasa basi naomba ujue ya
kwamba hakuna mema yoyote pasipo neno, mtu mwingine anaweza akajiuliza
maswali mengi akakosa majibu, ila ndugu
yangu ngoja tu nikueleze ya kwamba, kila unachokitafakari sana ndicho mara
nyingi unachokipata sasa na baadae. Sasa basi ni bora sana tena sana wewe uamue
leo kutafakari neno la Mungu lenye pumzi ya uhai ili upate mema yote yaliyozungumzwa humo (yaani
kwenye biblia),
JE NI KWELI TUKISOMA NENO, TUNAMSOMA
YESU?
Ndio hii ni kweli kabisa! Tukisoma neno twamsoma
YESU!, yaani tukisoma neno tunamsikia YESU anavyotuagiza juu ya maisha yetu,
kwa sababu YESU ni NENO. Ha! Hii ni kweli jamani!? Ninajua ni jinsi gani
unavyojiuliza maswali mengi ambayo yanakusumbua kupata majibu yake mara moja,
ila mimi nikwambie ya kwamba kwa kuwa ROHO MTAKATIFU ni msaidizi wako naye yupo
nawe hapo wakati unatafakari kitabu hiki, ninajua atakusaidia kuyaelewa haya.
Sasa basi hebu twende kwa kuyaangalia kiundani
maneno ya Mungu, Roho mtakatifu akitusaidia. JE NDUGU YANGU UPO TAYARI TUANZE?
Haya hebu fungua kitabu cha yohana
1:1-5. Utakuta maneno haya “hapo mwanzo kulikuwepo Neno, naye Neno alikuwa
kwa Mungu, naye Neno alikuwa Mungu. ……………………………………………”,
haya hebu turuke na tusome yohana 1:14,
ambapo utakuta maneno haya “naye Neno alifanyika mwili. Akakaa kwetu: nasi
tukauona utukufu wake, utukufu kama wa mwana
pekee atokaye kwa Baba; amejaa neema na kweli”. Hivi ndugu yangu, je ni
nani aliyefanyika mwili akakaa kwetu?, ni nani mwana pekee wa Baba?, je YESU
siye NENO ambaye alikuwa MUNGU?. YESU ndiye NENO kutokana na maandiko ya yohana
tuliyoyasoma. Ndugu mpendwa mimi ninajua ya kwamba Roho mtakatifu kwa wema wake
amekufundisha vizuri kabisa Nawe umeelewa vema.
Lakini ndugu
yangu hebu pata shauku ya kuendelea kuyachunguza maandiko na kuyatafakari zaidi
ili Roho mtakatifu msaidizi wetu mwema azidi kusema nawe kiundani zaidi kwa
sababu MUNGU huwapenda watu wachunguzao maandiko kila siku, soma matendo 17:11 “watu hawa walikuwa
waungwana kuliko wale wa thethalonike, kwa kuwa walipokea lile neno kwa ulekevu wa moyo, wakayachunguza maandiko kila siku, waone
kwamba mambo hayo ndivyo yalivyo.” Sasa
basi hebu nawe zingatia kuyachunguza maandiko KILA SIKU ili upate kuelewa
kiundani MUNGU anasema nini nawe.
Angalia tena ufunuo
19:13-16 ”naye amevikwa vazi lililochovywa katika damu, na jina lake aitwa,
NENO LA MUNGU ……………………………………………………………………………… naye ana jina limeandikwa katika
vazi lake na paja lake, MFALME WA WAFALME, NA BWANA WA MABWANA.” Je ni nani aitwaye MFALME WA WAFALME?, tena
ni nani aitwaye BWANA WA MABWANA?. Ninajua utakuwa haujapishana sana na ukweli,
na pia jibu lako litakuwa ni “YESU”. Sasa basi hebu rejea mstari wa 13b NA JINA
LAKE AITWA, NENO LA MUNGU. Sasa nadhani umeelewa ya kwamba ukisoma NENO
unamsoma YESU moja kwa moja.
Ndugu yangu kutokana na jinsi tulivyoona hapo juu na
jinsi Roho mtakatifu anavyozidi kukukumbusha naomba uamini sasa kwa jina la
YESU kristo wa nazareti aliye hai jina lipitalo majina yote, ya kwamba
“Unavyopata muda wa kutafakari Maneno ya Mungu (Biblia), unapata muda wa
kumsikiliza YESU mwenyewe anasema nini kwenye maisha yako. Na ukitenda sawa
sawa na maneno ya Biblia takatifu (neno la Mungu), utakuwa unatenda sawa sawa
na YESU anavyotaka wewe utende.
Ndugu yangu kumbuka kusoma neno! Kutafakari neno! Na
kutenda neno, Kwa maana nyingine utakuwa unamsoma yesu anavyokuagiza ndani
yako! Kisha unamtafakari yesu! Halafu unatenda Kama yesu anavotaka utende,
ELEWA YA KWAMBA ukizingatia neno la Mungu utapata kufanikiwa na kusitawi sana,
kwa sababu hakuna jambo lolote chini ya jua ambalo halipo kwenye neno la Mungu,
Kila kitu kipo kwenye neno la Mungu.
Shetani anafanya kila jitihada kuhakikisha kwamba
wewe husomi neno na ukisoma huelewi na ukielewa hutendi kama neno
linavyokuagiza, kwa sababu anajua MAFANIKIO YAKO YAPO KWENYE NENO LA MUNGU.
Ndugu yangu SOMA NENO, TAFAKARI NENO, TENDA NENO!
Nawe utapokea vingi kutoka kwa BWANA, elewa kwamba NENO ndilo pekee litasimama
mambo yote yatapita lakini neno tu ndilo litadumu, Kwa maana nyingine YESU
pekee atasimama. Soma 1Petro 1:23-25
NINI
HASARA YA KUTOSOMA, KUTOTAFAKARI NA KUTOTENDA NENO ?
- UTAANGAMIA KIROHO NA KIMWILI
Ukisoma Hosea 4:6 utakutana na maneno “watu
wanguwanaangamizwa kwa kukosa maarifa; kwa kuwa wewe umeyakataa maarifa, mimi
nami nitakukataa wewe, usiwe kuhani kwangu mimi; kwa kuwa umeisahau sheria ya
Mungu wako, mimi nami nitawasahau watoto wako”, sasa hapa ndugu yangu unaweza
kugundua kitu kimoja ya kwamba Mambo ambayo walizuiliwa yalitokana na wao
kukosa maarifa na ambayo yalizungumzwa kwamba yatokana na Neno la Mungu kama mistari ya mwanzo kabisa ya hosea katika
sura ya nne inavosema “lisikieni NENO la BWANA,………………………..” unaweza ukagundua
ya kuwa kuangamia kwa watu wake Mungu kunatokana na kutokulisikia neno la
BWANA, kwani ukiendelea kuangalia mistari ya mwanzoni kabisa inayoendelea hapo
chini katika sura ya nne utaona kuwa kwa kutokulisikia neno la BWANA nchi
iliingia katika dhambi kama “kuapa kwa uongo, na kuvunja ahadi, na kuua, na
kuiba, na kuzini…………”, sasa ukijaribu kuanzalia kitabu hiki cha Hosea utaona ya
kwamba nchi ile ilitenda dhambi sana, hasa hasa dhambi ya uzinzi na iliacha
kusikia neno la bwana, ndio maana BWANA akawasikitikia kwa kuangamia kwao kwa
sababu yeye hapendi watu wake waangamie ndio maana akaamua kumtuma Yesu kristo
mwana wake wa pekee ili kila amwaminiye asipotee bali awe na uzima wa milele (yohana 3:16), sasa basi hebu jaribu
tena kuangalia katika mstari wa sita wa hosea kwa makini kisha uutafakari
kiundani ukimwomba Roho Mtakatifu akusaidie, ukiutafakari vizuri utagundua ya
kwamba ukikataa maarifa ya Mungu, MUNGU ATAKUKATAA PIA, KISHA ATAWASAHAU WATOTO
WAKO; sasa angalia hasara ya kutotafuta maarifa ya BWANA kupitia NENO LAKE
TAKATIFU(BIBLIA), yaani kukataliwa kutaanza kwako wewe kwanza kisha kutaendelea
mpaka kwa watoto wako! Ndio sijakosea namaanisha ya kwamba, kutaendelea mpaka
kwa watoto wako.
Hebu jiulize swali
lifuatalo ndugu yangu, “Hivi haya mambo yaliyowasababisha watu wa Mungu waangamizwe
je hayapo kwenye amri kumi za Mungu?”, jibu ni rahisi tu ndugu yangu, mambo
hayo yote yameandikwa kwenye amri kumi. Hebu soma mwenyewe kitabu cha Kutoka 20:1-17 na kumbukumbu 5:6-21. Hebu tujiulize tena sasa “hivi kama amri zipo
na watu wanaangamizwa na kama neno lipo na watu wanaangamizwa, maana yake ni
nini?”. Maana yake ni kwamba watu wenyewe wanataka kuangamizwa kutokana na ukweli kwamba neno la Mungu
limewekwa wazi kwa kila mtu anayetaka kulijua na kila mtu anayetaka kufanikiwa
na kusitawi (yoshua 1:8).
Shetani baba wa uongo
anajitahidi sana kukudanganya ili usipate muda wa kusoma neno na kutafakari
neno, kwa sababu anajua silaha mojawapo ya mafanikio yako kimwili na kiroho ni
NENO LA MUNGU, soma waefeso 6:17b
“na upanga wa Roho ambao ni neno la Mungu”. Hivi wewe unafikiri shetani ni
mjinga sana eeh! Eti akuachie tu wewe uwe na UPANGA WA ROHO ili umkate na
kumuua kabisa, hapana ni lazima apigane nawe kwa kiasi kikubwa na ahakikishe ya
kwamba hupati muda hata kidogo wa kuangalia neno la Mungu. Naomba utambue ya
kwamba mafanikio yako ya kimwili yanaanza na mafanikio yako ya kiroho, soma mwenyewe
3Yohana 1:2 utakuta maneno haya
“mpenzi naomba UFANIKIWE katika mambo YOTE na kuwa na afya yako, kama vile roho yako IFANIKIWAVYO”, sasa ukubali
ukatae hii ni kanuni ya kiMungu ya kwamba, unataka ufanikiwe katika mambo yote
na kuwa na afya yako (kimwili) ni lazima uanze kutakuta kuwa na mafanikio
kiroho kwanza, kwa hiyo kama unataka shetani asikushinde katika mambo yote ni
lazima utafute kwanza UPANGA WA ROHO yaani NENO la Mungu, tena sio utafute tu
likae kinywani mwako, ulitafakari naulitende (yoshua 1:8), ooooh HALELUYA mtu
wa Mungu!, Nakusihi usiache kuyatendea kazi haya maneno ambayo Roho anakuambia
hivi sasa.
- HUTAPATA MAJIBU YA MAOMBI YAKO
Mtu mwingine anaweza
asikubalie kabisa na jambo hili na wala asielewe kabisa kwamba majibu ya maombi
yote ayaombayo hutokana na jinsi gani mtu amelijaza neno la Mungu ndani yake,
najua suala hili limekuwa likikusumbua kwa kiasi kikubwa kwani hata mimi
lilinisumbua sana, lakini ninamshukuru Yesu wangu kwa wema na fadhili zake
kwani aliamua kunifundisha yeye mwenyewe kupitia uwezo wa Roho Mtakatifu ambaye
ndiye msaidizi wetu, ndio maana leo ameamua kukufundisha na wewe ili ukiomba
upokee majibu yako pasipo na shaka yoyote, ila kabla hatujaangalia maandiko
nasikia roho mtakatifu akinikumbusha nikwambie ya kwamba majibu ya maombi yako
hayatatokana tu na kulijaza neno pekee bali kulitenda na kuzingatia maagizo
akupayo msaidizi wako Roho Mtakatifu.
Sasa hebu tuangalie
kitabu cha Yohana 15:7 ambapo
tutakutana na maneno yafuatayo”ninyi mkikaa ndani yangu, na MANENO YANGU yakikaa
ndani yenu, OMBENI mtakalo lote nanyi MTATENDEWA”, ndugu yangu katika jina la
Yesu kristo wa nazareti aliye hai ninamwomba Roho Mtakatifu akusaidie upate
kuelewa vizuri na akuwezeshe ili macho yako ya rohoni yapate kutiwa nuru kabisa
na ujue kusudi la Mungu kuweka kitabu hiki mbele yako.
Sasa hebu tutafakari
kwa pamoja maneno haya ya Mungu yaliyoandikwa katika kitabu cha Yohana mtakatifu,
utaona Yesu anasema ya kwamba “ninyi mkikaa ndani yangu”, yaani wewe ndugu
yangu msomaji ukikaa ndani ya Yesu kabisa kabisa na ukijitoa kuwa mali ya Yesu
yaani UKIOKOKA, na situ kuokoka pekee bali ukitenda kama Yesu anavyokuagiza
utende, basi utajibiwa maombi yako pasipo shaka yoyote.
Kwa sababu ni lazima
uelewe ya kwamba huwezi kukaa ndani ya YESU halafu eti bado Ukawa MZINZI,
MLEVI, MCHAWI, FISADI na namna nyingine mbaya ambazo unazo na Roho Mtakatifu anakushuhudia
ya kwamba ni mbaya. Hebu soma mwenyewe Wagalatia
5:19-21 utayaona matendo ambayo ukiwa nayo huwezi kukaa ndani ya Yesu.
Lakini ukiwa na matendo
mema kama UPENDO,FURAHA,AMANI na mengine mengi mazuri kama yalivyoandikwa
katika kitabu cha Wagalatia 5:22-23 utakaa
ndani ya yesu na kupata manufaa mengi ambayo yapo kwa Yesu kristo wa nazareti
aliye hai, Acha tu nikwambie ndugu yangu ya kwamba ukiwa ndani ya Yesu unapata
uwezo wa kufanyika mwana wa Mungu (yohana1:12), pia unakuwa rafiki wa Yesu (yohana 15:14-15) na zaidi sana Roho
mtakatifu anapata kibali cha kukaa ndani yako na kukusaidia katika mambo yote (1wakorintho 3:16).Sasa wewe unasubiri
nini kumpokea Yesu? Mimi nakushauri amua sasa kumpokea Yesu ukimaanisha kabisa
kutoka ndani ya Roho yako, na kufuata sala ambayo itakuwa mwishoni kabisa mwa
kitabu hiki kwa uwezo wa Roho mtakatifu.
Ila sasa kumbuka ya
kwamba Yesu hakuishia tu kusema maneno“ninyi mkikaa ndani yangu” pekee, bali
aliendelea tena kwa kusema “na maneno yangu yakikaa ndani yenu, ombeni mtakalo
lote nanyi mtatendewa”, sasa ni lazima uelewe ya kwamba, kutendewa kwako katika
hayo maombi unayoomba kunatokana kabisa na kuyaweka maneno ya Mungu kwa wingi
ndani yako, ndio maana akasisitiza “na maneno yangu yakikaa ndani yenu” halafu
akamalizia “ombeni mtakalo lote mtatendewa”.
Sasa mimi binafsi
nakushangaa wewe usiyetaka kusoma, kutafakari na kutenda neno la Mungu halafu
unatarajia majibu ya maombi yako, ndio eeh! Mimi nakushangaa kabisa kabisa,
halafu baada ya kukushangaa naona ni vema nikushauri ili watu wengine wasikushangae
sana, na ushauri wangu kwako ni kwamba “SOMA NENO, TAFAKARI NENO, TENDA NENO”, halafu
uone kama hujajibiwa maombi yako!, mimi nakuhakikishia kwa jina la Yesu kristo
wa nazareti aliye hai ya kwamba ni lazima ujibiwe hayo maombi yako, kwa sababu
mimi binafsi nilijibiwa na na naendelea kujibiwa mengi niliyoyaomba baada ya
kugundua kanuni hiyo.
- UTALAANIWA
“Na alaaniwe
asiyeyaweka imara maneno ya torati hii kwa kuyafanya. Na watu wote waseme,
amina ”,Kumbukumbu 27:26, ukijaribu
kuyachunguza vizuri maneno haya ambayo yameandikwa kwenye kitabu cha tano Musa
cha kumbukumbu la torati. Utagundua ya kwamba, Mungu alipenda kuwapa maagizo
wanaisraeli moja kwa moja kupitia mtumishi wake musa, ili kwa yeyote
atakayetaka kuyafuata maagizo ya Mungu basi awe salama, na kwa atakayekaidi
apate ujira wake wa laana pia.
Sasa hebu sikia maneno
haya na uyatafakari kwa makini, “na alaaniwe!”
Mmh! ndugu yangu, hebu tujiulize ni nani alaaniwe?. “Asiyeyaweka imara
maneno ya torati!”. Eeeh! Kumbe usipoyaweka imara maneno ya torati ni wazi
kwamba unataka laana, sasa utayawekaje imara maneno ya torati? Jibu ni kwa
kuyafanya, Aaah kumbe! Ili nisilaaniwe inabidi niyafanye yale Bwana aniamuruyo,
unaweza kwenda mbali kidogo kwa kusema ya kwamba, ili mtu apokee Baraka ni
lazima, ndio nasema ni lazima namaanisha ya kwamba sio ombi!, NASISITIZA NI
LAZIMA ASOME NA KUTENDA SAWA SAWA NA NENO LA MUNGU.
Sasa kwa kuwa neno la
Mungu lina umuhimu sana basi Musa alipokufa tu, Mungu aliendelea kumkumbusha
hata Yoshua juu ya umuhimu wa kuzingatia maneno yake, ili asitawi katika maisha
yake na kuepuka laana kabisa, sasa unaweza ukajua kwamba Baraka zilizomiminika
kwa wana Israeli zinatokona moja kwa moja na kutunza na kufanya maagizo ya
BWANA Mungu, soma mwenyewe Kumbukumbu
28:1-14.
Sasa ukisikia Mungu
anazungumza jambo na wewe halafu unakaidi kutenda, utakuwa unatafuta matatizo
wewe mwenyewe, yaani ukisikia Mungu anasema utalaaniwa kwa kutokuweka imara
torati yake, inamaanisha kuwa utalaaniwa kweli kweli, sasa basi wewe ukielewa
hivyo tu, unatakiwa uweke imara torati ya BWANA Mungu wako ili ubarikiwe na
usilaaniwe. Kumbuka kanuni yetu ya muhimu kabisa na rahisi sana
itakayokuwezesha kupokea Baraka “SOMA NENO,TAFAKARI NENO,TENDA NENO”.
- UTAKUFA KIROHO NA KIMWILI
Labda nianze kwa
kukuweka sawa ya kwamba, kanuni ni kwamba ukitaka kufa kimwili basi anza kwanza
kuua Roho, na ukitaka kufanikiwa kimwili anza kutafuta kufanikiwa kiroho kwanza,
ninajua kwa sasa unaweza usielewe namaanisha nini. Lakini kwa kuwa Roho
Mtakatifu ni mwema mimi ninajua ya kwamba atakupitisha kwenye shule hii
kiurahisi kabisa. Haya sasa je! Ndugu upo tayari tufundishwe sote na Roho
Mtakatifu?
Haya tuanze shule yetu
kwa uwezo wa Roho Mtakatifu sasa kwa kusoma 3 yohana 1:2, utakuta maneno yafuatayo “mpenzi naomba ufanikiwe
katika mambo yote na kuwa na afya yako, kama vile roho yako ifanikiwavyo”, haya
sasa! Najua umeanza kupata picha kidogo kwamba namaanisha nini, Ni wazi kabisa
kwamba utafanikiwa kwa kadiri au kwa kiwango cha mafanikio ya roho yako, sasa
kama roho yako inafanikiwa kidogo na mwili pia utafanikiwa kidogo, kama roho
yako itafanikiwa sana na mwili pia kadhalika. Na tena kama roho yako itaishi na
mwili pia utaishi, sasa basi! ujue kwamba roho yako ikifa na mwili wako utakufa
tu.
Hebu sasa tuyaangalie
maneno ya kitabu cha Mathayo 4:4 ambayo
yanasema “naye akajibu akasema, imeandikwa , mtu hataishi kwa mkate tu, ila kwa
kila neno litokalo katika kinywa cha Mungu.”
Sasa najua utaelewa ya kwamba kuishi kwako kutatokana na jinsi
ulivyolijaza neno la Mungu ndani yako, kadhalika kufa kwako kutatokana na
kutolijaza neno la Mungu ndani yako.
Hivi unafikiri Yesu
asingelikuwa na neno ndani yake angemjibu kwa kusema imeandikwa! Hebu jiulize
imeandikwa wapi? Halafu fikiri kwa nini Yesu alisema hakuja kuitangua torati
bali kuitimiza. Sasa utaelewa ya kwamba mwana mpendwa wa Mungu, yaani Yesu
mwenyewe aliishi kwa kuzingatia na kutenda neno, sasa kwa nini wewe usitende neno?
Ndugu yangu mpendwa,
mimi ninakushauri ujitahidi kujua neno la Mungu, ili shetani asikutishe na
kukuletea uongo wake kabisa. Kwa mfano akikujaribu katika masomo ya kwamba
utafeli, wewe ungali ukijua neno la Mungu umwambie kwa ujasiri wote ya kwamba “
imeandikwa kwenye kumbukumbu 28:13,
ya kwamba BWANA atanifanya kuwa kichwa na wala sio mkia;………., kwa hiyo ni
lazima nifaulu katika jina la Yesu”, akikujaribu kwenye Ndoa umwambie imeandikwa katika mithali 18:22 ya kwamba “apataye mke apata kitu chema; naye
ajipatia kibali kwa BWANA, kwa hiyo mimi
nimepata mke au mume mwema kabisa kabisa katika jina la Yesu”, akikwambia wewe
ni maskini umwamie “imeandikwa katika wafilipi
4:19 ya kwa Mungu atanijaza kila nachohitaji kwa kadiri ya utajiri wake,
kwa hiyo mimi ni tajiri katika jina la Yesu”. Sasa kwa nini uteseke na Yesu yupo? Tena anakupenda na
kukujali?, wewe jitahidi tu kusoma neno na kumwomba yeye, naye hakika
atakusaidia.
Hebu na tusome kwa
kutafakari Mithali 4:20-22, Isemayo
“mwanangu, sikiliza maneno yangu; tega sikio lako, uzikie kauli zangu.
Zisiondoke machoni pako ; uzihifadhi ndani ya moyo wako. Maana ni UHAI kwa wale
wazipatao, na afya ya mwili wao wote.”, nadhani umejionea mwenyewe hilo neno ni
UHAI kwa wale wazipatao, na afya ya mwili wao wote. Sasa ni lazima uelewe
kwamba mithali hii ya sulemani ina maana kubwa sana kwako mtu wa Mungu, ya
kwamba ni lazima uyasikilize maneno ya Mungu, halafu utege sikio usikie kauli
za BWANA, halafu tena zisiondoke machoni kwako kabisa bali uzihifadhi, hebu
jiulize, je uzihifadhi wapi?, Ni rahisi kabisa uzihifadhi ndani ya moyo wako,
Kwa tafsiri nyingine uhai wako unategemea neno la Mungu.
Ndugu yangu usisahau
kanuni yetu ya mambo yote! SOMA NENO, TAFAKARI NENO, TENDA NENO, ili upate uhai
wako na usife kwa kukosa kuifahamu kweli ya Mungu wetu.
- UTATENDA DHAMBI
Soma mwenyewe Zaburi 119:11, ambapo neno la Mungu
linasema “moyoni mwangu nimeliweka neno lako, nisije nikakutenda dhambi”, ngoja
tujiulize kwa pamoja kabisa, hivi ni kwa nini neno katika zaburi
halikusema ya kwamba, “moyoni mwangu
nimejaza maombi nisije nikakutenda dhambi, au moyoni mwangu nimezijaza sifa
zako nisije nikakutenda dhambi, au moyoni mwangu nimejaza ibada nisije nikakutenda dhambi, au “moyoni mwangu
……………………………. Nisije nikakutenda dhambi?”
Jibu ni rahisi kabisa
mtu wa Mungu ni vema ufahamu ya kwamba neno ni msingi wa kila kitu katika
maisha yako, ukitaka kuomba vizuri lazima ujue neno linasemaje juu ya maombi (yohana 15:7), tena ukitaka kusifu
vizuri ni lazima ujue neno linasemaje kuhusu sifa (waebrania 13:15), tena ukitaka ibada nzuri ni lazima ujue neno la
Mungu lasemaje kuhusu ibada (yohana
4:23-24), tena ukitaka …………… tafuta kwanza neno la Mungu linasemaje kuhusu
………….. na utende.
Sasa ni lazima umwombe
Roho Mtakatifu akusaidie na wewe uweze kuliweka neno la Mungu ndani yako ili tu
usije ukamtenda Mungu dhambi, ndio eeh! Lazima umwombe Roho Mtakatifu akusaidie
kwa sababu vita iliyopo juu ya kusoma neno ni kubwa sana, Shetani hataki kabisa
wewe ujue neno kwa sababu atakukosa katika orodha yake ya kwenda jehanamu.
Ndugu jitahidi ujue
neno la Mungu ili uepuke mshahara wa dhambi ambao ni mauti (warumi 6:23), sasa kama unataka mauti,
kazi ni rahisi sana, wewe jitahidi kutojua neno la Mungu ili utende dhambi. Ila
kama unataka uzima wa milele, pia kazi rahisi SOMA NENO, TAFAKARI NENO, TENDA
NENO.
NINI FAIDA YA KUSOMA, KUTAFAKARI NA KUTENDA NENO?
1. YESU
ATAKUOMBEA
Ukisoma katika kitabu
cha Yohana 17:8-9 utakuta maneno
yafuatayo “kwa kuwa maneno uliyonipa
nimewapa wao; nao wakayapokea, wakajua hakika ya kuwa nalitoka kwako,
wakasadiki ya kwamba wewe ndiwe uliyenituma. Mimi nawaombea hao; siuombei ulimwengu; bali hao ulionipa, kwa kuwa hao
ni wako ”, Sasa unaweza ukatambua ya kwamba ukilipokea neno la Mungu basi
Yesu mwenyewe atakuwa akikuombea,
ukiangalia katika mistari ya kwanza kabisa ya mlango huu wa 17 utagundua ya
kwamba Yesu aliomba maombi haya katika wakati ambao alikuwa anakaribia kabisa
kuteswa na kufa kwa ajili ya wanadamu wenye dhambi.
Sasa unaweza ukajiuliza
ni kwa nini asingeomba tu kwa ajili ya ulimwengu mzima katika maombi yake
haya!, bali akaanza kwa kusema maneno
uliyonipa nimewapa wao nao wakayapokea, halafu akasema katika mstari wa 9 mimi nawaombea
hao. Sasa namwomba roho mtakatifu ayafungue macho yako upate kuelewa na
maandiko (luka 20:45), ya kwamba
kama hutaki neno Yesu hawezi kujiangaisha na wewe, ila kama ukijaza neno lake
ndani yako; uelewe kabisa ya kwamba atakuombea.
ukiendelea tena mbele kidogo na kusoma kitabu
cha yohana 17:14-15 utakuta Yesu
akiendelea kusema “mimi nimewapa neno
lako; na ulimwengu umewachukia; kwa kuwa wao si wa ulimwengu, kama mimi
nisivyo wa ulimwengu. Mimi siombi
kwamba uwatoe katika ulimwengu; bali uwalinde na Yule mwovu. ” naomba uelewe
kwamba, Mambo haya sio ya kawaida kawaida, ukae ukijua ya kwamba ukilitambua
neno la Mungu wa kweli ni lazima uchukiwe!, kama hutaki kuamini hebu anza leo
kuishi sawa na neno la Mungu. Halafu uone kama hujachukiwa na wale rafiki zako
uliokuwa ukienda nao disco, tena kama hujachukiwa na Yule uliyekuwa unazini nae
kabla ya kujua neno, halafu kama hujachukiwa na Yule ulikuwa ukishinda nae bar,
tena zaidi sana kama hujachukiwa na Yule ulikuwa ukienda nae kwa mganga ili
umfanyie madawa mumeo. Mimi nakwambia utachukiwa sana; lakini ukae ukitambua ya
kwamba thamani yako itapanda kwa kuwa Yesu mwenyewe atakuombea, halafu Yule
mwovu hatakuweza tena katika jina la Yesu kristo wa nazareti aliye hai.
Je unataka Yesu
mwenyewe akuombee kila mara?, usisahau ya kwamba kanuni yetu ambayo Yesu
ametupa sisi kupitia kwa Roho Mtakatifu ni ndogo tu! SOMA NENO, TAFAKARI NENO,
TENDA NENO.
2. UTAIJUA
KWELI, KISHA UTAKUWA HURU
Ukisoma katika kitabu
cha Yohana 8:31-32 utakuta maneno
haya “ basi Yesu akawaambia wale wayahudi wasiomwamini, ninyi mkikaa katika neno langu, mmekuwa
wanafunzi wangu kweli kweli; tena mtaijua
kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru”, tena
ukisoma katika kitabu cha Yohana
17:17 utakuta maneno yafuatayo “uwatakase kwa ile kweli; neno lako ndiyo kweli”
Bila shaka kutokana na
maneno tuliyosoma utakuwa umepata kuelewa ya kwamba; neno la Mungu ndiyo kweli
itakayokusaidia kiroho na kimwili. Ukitaka kuwa huru kabisa katika mambo yote
maishani mwako, kanuni ni ndogo tu SOMA NENO,TAFAKARI NENO, TENDA NENO.
Sasa kama hutaki kuishi
katika kweli maana yake unataka uwe katika vifungo, na ninakuhakikishia shetani
hatakuachia hata siku moja kwa kwenda kwako kanisani pekee, au kuimba kwaya
pekee, au kuwa shemasi pekee, au hata kuwa mwinjilisti au mchungaji. Shetani
atakuachia na utakuwa huru kweli kweli pindi tu utakapoijua kweli ambayo ni neno
la Mungu wa mbinguni (biblia yaani maandiko matakatifu).
Mimi nakushauri
ujitahidi kwa kadiri uwezavyo ili tu uwe msomaji wa neno, halafu usiishie tu
kulisoma bali ulitafakari, zaidi sana ukalitende. Kisha upokee uhuru wako
katika mambo yote maishani mwako.
3. UTAFANIKIWA
NA KUSITAWI SANA
Hii ni wazi kabisa
kwamba; mafanikio yako na usitawi wako, vipo kwenye neno la Mungu, unaweza
usielewe kirahisi sana lakini najua Roho Mtakatifu atakusaidia uelewa wako na
Yesu atafungue macho yako ili uone anakuwazia nini pindi tu upatapo kulijua
neno lake. Sasa tukisoma katika kitabu cha Yoshua
1:8 utakuta Mungu anamwambia Joshua ya kwamba “kitabu hiki cha torati
kisiondoke kinywani mwako, bali YATAFAKARI maneno yake mchana na usiku, upate
kuangalia KUTENDA sawasawa na maneno yote yaliyoandikwa humo; ndipo
UTAKAPOIFANIKISHA njia yako, kisha ndipo UTAKAPOSITAWI sana.
Lazima uelewe ya kwamba
mafanikio yako yote yataletwa na wewe kufahamu neno la Mungu, bila neno hakuna
mafanikio. Mimi nakwambia ya kwamba Mungu anaangalia neno lake alitimize (yeremia 1:12b), halafu anataka
umpelekee hoja zenye nguvu, halafu anataka ueleze mambo yako upewe haki yako (isaya 43:26).
Hivi unafikiri unaweza
kudai haki usiyojua kama ni yako? Au unaweza kuomba kitu pasipo na kujua kama
kipo? Au? Au? Najua maswali ni mengi sana, tena mengine na wewe unayo. Lakini
neno la Mungu limeweka wazi kabisa suala hili; kwamba Mungu huliangalia neno
lake ili alitimize (yeremia 1:12b),
sasa kama huna neno la Mungu unafikiri ni kitu gani kitatimizwa kwako?
Lazima uelewe kwamba
mafanikio yako yanakuja kwa kulifahamu neno la Mungu, kwa mfano; unataka mke
mwema, mithali 18:22 ipo wazi kabisa
kwamba apatae mke apata kitu chema. Sasa wewe unapokwenda kwa Mungu kuomba
pasipo kujua neno hili, ujue ya kwamba maombi yako yatakuwa kelele kwa Mungu,
kwa sababu Mungu anaangalia neno lake ili alitimize, unataka mafanikio yako ya
mbeleni yawe mazuri, Isaya 45:11 ipo
wazi kabisa Mungu anataka umuagize juu ya mambo yanayokuja, sasa wewe
unapokwenda kwa Mungu kuombea maisha yako yajayo pasipo na kujua neno hili;
ujue utapiga kelele bure kwa Mungu, halafu yeye ashakwambia anaangalia neno
lake ili alitimize, si hayo tu neno la Mungu lina majibu ya kila unachokifahamu
hapa chini ya jua.
Kwa hiyo unataka
kufanikiwa na kusitawi kanuni tuliyopewa ni ndogo tu; SOMA NENO,TAFAKARI NENO
,TENDA NENO. Vinginevyo usahau tu kuhusu mafanikio kwa sababu shetani atakuwa
amekufunga kisawasawa na kwa kuwa anachukia usitawi wako hutafanikiwa. Lakini
kwa jina la Yesu kupitia Roho Mtakatifu wake ambao leo, wamekupa wewe kibali
cha kusoma kitabu hiki ninamuamuru shetani aachie fahamu zako ili upate kupokea
kile mungu anachokuwazia (yeremia 29:11)
katika jina la Yesu kristo wa nazareti aliye hai.
4. UTAMSHINDA
SHETANI
Hebu tujiulize swali
hili kwa pamoja kabisa, Je utamshindaje shetani? Ni rahisi kabisa ukisoma
katika kitabu cha waefeso 6:10-20,
utakuta mtume Paulo anawaandikia watu wa efeso kwamba wanatakiwa wawe hodari
katika bwana na katika uweza wa nguvu zake, kisha wavae silaha zote za Mungu
ili waweze kuzishinda hila za shetani; Kwa maana kushindana kwetu si juu ya
damu na nyama bali juu ya falme na mamlaka. Sasa ukiangalia kuanzia mstari wa
14 mpaka wa 20 utakuta zimerodheshwa silaha za kuweza kumpinga shetani na
kumshinda kabisa kabisa. Mimi nakushauri uzisome na kuangalia kutenda sawa sawa
na neno hili la Mungu ili uweze kumpinga shetani
Kwa hiyo ukisoma Waefeso 6:17b utakuta maneno haya “na upanga wa Roho ambao
ni neno la Mungu” kumbuka kuanzia mstari wa 14 mpaka wa 20 zilikuwa
zinazungumziwa silaha za Mungu, sasa neno ni upanga wa Roho; kwa maana nyingine
neno linao uwezo wa kumkata kata shetani na serikali yake yote ya kuzimu.
Sasa kama neno ni
upanga na wewe hujui neno, tena hutaki kulijua kabisa kabisa, na hata ukipata
neema ya kulijua hutaki kulitumia (kulitenda) maishani mwako, unategemea nini?,
jibu ni rahisi kabisa nalo ni!, utake
usitake ni lazima shetani atakushinda kwa sababu akiangalia rohoni mwako kama
kuna upanga utakaoweza kumpinga hauoni, Na asipouna anakuangamiza wewe ili
usije ukajua neno (upanga wa Roho) halafu ukamteketeza.
Nikushauri tu ndugu
yangu mpendwa ya kwamba, Upanga huu wa Roho hauna gharama yoyote kuupata,
ingawa shetani anajaribu kukurubuni usiutafute na kuutumia. Amua hivi sasa
kumpokea Yesu kwanza kama bado hujampokea kwa kufuatisha sala ambayo utaikuta
mwishoni mwa kitabu hiki, kisha umwombe Yesu wewe mwenyewe kwa kinywa chako
akusaidie kupitia Roho Mtakatifu, uweze kuelewa maandiko na upate hamu ya
kuijua kweli ili uwe huru, na umshinde shetani kabisa kabisa.
5. UTAPATA
NGUVU YA MUNGU
Katika 1Wakorintho 1:18, neno la Mungu
linasema “ kwa sababu neno la msalaba kwao wanaopotea ni upuuzi, bali kwetu
sisi tunaookolewa ni nguvu za Mungu.” Sasa usije ukatafsiri kama wengi
wanavyotafsiri, maana wengi hudhani imeandikwa hivi, “kwa sababu neno msalaba”
hapana haijaandikwa kwa sababu neno msalaba, bali imeandikwa kwa sababu neno la
msalaba, je neno la msalaba ni lipi? Ukisoma katika kitabu cha 2 wakorintho 4:3 utakuta neno hili
limejaribu kuelezewa kwa namna nyingine kwamba, “lakini ikiwa injili yetu
imesitirika, imesitirika kwa hao wanaopotea”. Najua pamoja na kutambua kwamba
neno la Mungu kwa sehemu nyingine limeelezwa kama injili, bado kuna wengine
hawajaelewa kabisa ni nini ninachokizungumzia hapa, haya hebu tuangalie warumi 1:16 ili tuone habari ya injili
hii, maneno ya Mungu yanasema “kwa maana siionei haya injili; kwa sababu ni
uweza wa Mungu uuletao wokovu, kwa kila aaminiye, kwa myahudi kwanza, na kwa
myunani pia”
Sasa najua umeanza
kupata picha ya kwamba, neno la msalaba ni nguvu za Mungu kwetu sisi
tunaookolewa, kwa maana nyingine kama hujaokoka huwezi kuwa na hizi nguvu za
Mungu, kwa sababu pia husomi neno. Najua wengine bado wanajiuliza maswali mengi
juu ya uhusiano wa neno la Mungu, neno la msalaba na injili, sasa ngoja Roho
mtakatifu atusaidie kutupa majibu, hivi kuna mtu ashawahi kuubiriwa injili kwa
kutumia kitabu cha siasa? Au basi kitabu cha hisabati? Au basi kwa kutumia
gazeti? Au kitabu cha hadithi? Au? Au? Au?.............., najua jibu lake ni HAPANA!
Haya sasa tujiulize tena, hivi mtu ashawahi kuubiriwa injili kutumia neno la
Mungu yaani maandiko matakatifu au kama inavyofahamia Biblia?, jibu lake ni
rahisi sana, au wewe unafikirije ndugu msomaji?, ila mimi nadhani jibu lake ni!
NDIO watu huubiriwa injili kwa kutumia neno la Mungu yaani Biblia.
Sasa utakubaliana na
maneno ya mtume Paulo katika 1wakorintho
1:18 kwamba, utapata nguvu za Mungu kwa neno la msalaba, lakini hakuishia
hapo ukiliona neno la msalaba ni upuuzi basi utapotea. Sasa amua leo, je
unataka kupotea au kupata nguvu za Mungu! Mimi binafsi nakushauri uamue kupata
nguvu za Mungu kwa kujua neno la msalaba. Na usiishie tu kulijua bali
ulitafakari na kisha ulitende, nakuhakikishia ya kwamba utaziona nguvu za Mungu
katika jina la Yesu.
6. UTAPATA
MWANGAZA KATIKA MAISHA YAKO
Katika Zaburi 119:105 maneno ya Mungu
yanasema hivi “neno lako ni taa ya miguu yangu, Na mwanga wa njia yangu”, je
taa yako na mwanga wa njia yako ni nini?, najua jibu unalo wewe mwenyewe,
pengine ni waganga, au pombe, au uongo au chochote ambacho unasikia Roho Mtakatifu akikukumbusha
ndani ya roho yako. Lakini katika maneno ya zaburi taa na mwanga wa mtu wa
Mungu ni neno la Mungu, sasa kama
wewe umeokoka halafu huna taa hii inayokuletea mwanga katika njia zako basi una
bahati mbaya sana. Ila mimi nikushauri katika jina la Yesu, uanze leo kuiwasha
taa ya neno la Mungu maishani mwako ili upate mwanga katika mambo yako yote.
Anza sasa,! kusoma, kutafakari na kutenda sawa na neno la Mungu, bado
hujachelewa!
ukisoma tena katika kitabu cha yohana 1:4-5 utakuta iimeandikwa “Ndani yake ndimo ulikuwamo uzima, nao
ule uzima ulikuwa nuru ya watu. Nayo nuru yang’aa gizani, wala giza
halikuiweza.”, unaweza ukajihoji ndani ya kitu gani kulikuwamo uzima, uliokuwa
nuru ya watu?, ni rahisi kabisa. Ni ndani ya neno ndimo kulikuwamo uzima, nao
uzima ulikuwa nuru ambayo haikuwezwa na giza kabisa. Ndugu yangu hebu tafuta
huo uzima katika neno, ili upate nuru na maisha yako yabadilike kabisa kabisa,
ili nawe upate mwangaza katika maisha yako bado hujachelea anza sasa kutenda
sawa sawa na maandiko.
tena ukisoma katika
kitabu cha waefeso 1:18-19 utakuta
maneno kwamba “macho ya mioyo yenu yatiwe nuru, mjue tumaini la mwito wake
jinsi lilivyo; na utajiri wa utukufu wa urithi wake katika watakatifu jinsi
ulivyo; na ubora wa ukuu wa uweza wake ndani yetu tuaminio jinsi ulivyo; kwa
kadiri ya utendaji wa nguvu za uweza wake;”, haya sasa macho yako yatatiwa nuru
gani zaidi ya neno?, hakuna nuru popote zaidi ya neno la Mungu, ukiangalia
vizuri katika waefeso 1:18-19 utagundua ya kwamba, huwezi kujua tumaini la wito
wake bila nuru ambayo ni neno, tena huwezi kujua utajiri wa urithi wake bila
kutiwa nuru itokanayo na neno, tena huwezi kujua ubora wa uweza wake ndani yako
bila kutiwa nuru itokanayo na neno; tena huwezi lolote lile unalolijua bila
neno.
Kwa hiyo sasa neno ni
msingi wa kila kitu kwa kila mwanadamu, ukitaka mafanikio na usitawi soma neno,
hutaki mafanikio na usitawi acha kusoma neno. Lakini mimi nimepata mafanikio
mengi na makubwa ambayo Yesu amenitendea mara tu baada ya KUSOMA NENO,
KUTAFAKARI NENO NA KUTENDA SAWA SAWA NA NENO.
KIPI BORA! FAIDA AU
HASARA?
Mmh! Mimi ntashangaa
sana kama utachagua hasara ambazo zipo nyingi kuliko hizo nilizoziandika hapo,
Roho Mtakatifu ameamua tuziangalie hasara hizo chache kwa undani. Ila
haimaanishi kwamba zipo hasara hizo tu, bali hizo ni chache alizoamua
kutufundisha, hivi kweli unaweza kuamua kuchagua kuangamia kiroho na kimwili?
Au kutopata majibu ya maombi yako? Au kulaaniwa? Au kufa kiroho na kimwili? Au
kutenda dhambi?, ninajua utakuwa umeitikia HAPANA. Sasa basi mbona bado hutaki
kusoma, kutafakari na kutenda neno?.
Haya sasa je! Upo
tayari kupata faida zinazotokana na kusoma, kutafakari na kutenda neno?. Mmh
Asante sana kwa jibu lako zuri! Sasa wewe ambaye upo tayari kuombewa na Yesu,
tena kuijua kweli ili uwe huru, halafu ufanikiwe na kusitawi, tena umshinde
shetani, na tena upate nguvu za Mungu, kisha upate mwangaza katika maisha yako.
Mbona hutendi sawa na maagizo ya neno la Mungu?
Mimi nakushauri leo
uchague faida, na umpokee Yesu. Lakini pia ukichagua hasara shauri yako
mwenyewe! Kwa sababu Yesu ameamua kukufundisha yeye mwenyewe kupitia Roho wake
mtakatifu, katika kitabu hiki. Mpokee Yesu leo upate faida mpendwa.
HITIMISHO
“basi atukuzwe yeye
awezaye kufanya mambo ya ajabu mno kuliko yote tuyaombayo au tuyawazayo, kwa
kadiri ya nguvu itendayo kazi ndani yetu”, waefeso
3:20, ninapenda kumshukuru Mungu kupitia mwanae Yesu kristo kwa msaada wa
Roho Mtakatifu wake kwa kuniwezesha kuandika kitabu hiki ambacho amekiweka
mkononi mwako ili kiwe msaada wako wa kiroho.
Ndugu mpendwa mimi
binafsi nakushukuru kwa kutoa muda wako mwingi sana na ulio na dhamani kubwa na
kuamua kukisoma kitabu hiki, lakini napenda nikwambie ya kwamba Mungu
amekuwezesha wewe kusoma kitabu hiki kwa mpango kamili kabisa, kwa kuwa yeye
anakuwazia mema siku zote (yeremia 29:11),
halafu alijua ya kwamba leo atakufungua macho ili upate kuelewa maandiko yake (luka 24:45), sasa mimi nikushauri kama
ulikuwa hujaokoka ni vema uchukue uamuzi leo wa kumpokea Yesu kama bwana na
mwokozi wako (yohaha 3:16-17,
warumi 10:10,13 na matendo 4:12)
kwa kusali sala fupi itakayofuata baada ya hitimisho hili huku ukimaanisha,
najua unaweza ukajiuliza swali hili, hivi ni kwa nini mimi ninakushauri wewe
uokoke? Jibu ni rahisi sana ndugu yangu, mimi ninakushauri uokoke kwa sababu
hutaweza kupata kibali cha kuyaelewa maandiko na kuishi maisha ya mafanikio na
usitawi bila msaada wa Roho Mtakatifu, na Roho Mtakatifu hawezi kukaa ndani
yako ukiwa bado ungali mwenye dhambi (1
wakoritho 3:16-17), hebu chukua hatua sasa ya kumpokea Yesu na uanze kuona
mafanikio na usitawi wako, hujachelewa chukua uamuzi wa kuokoka hivi sasa; Kwa
kutafuta mahali penye utulivu na kusali sala ifuatayo kwa sauti kabisa huku
ukimaanisha, tambua ya kwamba Yesu yupo nawe hapo ulipo, halafu tena yupo
tayari kukusamehe na kukupokea kisha akufanye kiumbe kipya.
SALA YA TOBA
Ndugu yangu Sali sala
ifuatayo kwa sauti kabisa huku ukimaanisha, haya sasa mpendwa hebu sema maneno
yafuatayo;-
“BWANA YESU, NINAKUJA
MBELE ZAKO HIVI SASA. NIMESIKIA SAUTI YAKO KUPITIA NENO LAKO TAKATIFU, YA
KWAMBA, NIZIACHE DHAMBI ZANGU ZOTE, NA NIKUFUATE WEWE YESU, ILI UNIBADILISHE
NIWE KIUMBE KIPYA, NIMEAMUA KWA DHATI KUTOKA NDANI YA MOYO WANGU, KUZIACHA
DHAMBI ZANGU ZOTE NA KUKUFUATA WEWE. NISAMEHE DHAMBI ZANGU ZOTE NA USIZIKUMBUKE
KABISA KAMA ULIVYOSEMA KATIKA KITABU CHA ISAYA 43:25, NISAFISHE KWA DAMU YAKO
NA UNIFANYE KIUMBE KIPYA. NIPE NA ROHO MTAKATIFU WAKO ILI ANISAIDIE KUISHI VEMA
KATIKA WOKOVU, SIKU ZOTE ZA MAISHA YANGU, AMEN.”
Hongera sana kwa uamuzi
uliouchukua hivi leo, ninapenda kukuhakikishia ya kwamba Mungu kupitia mwanae
Yesu kristo amekusamehe dhambi zako zote, hajakusamehe dhambi baadhi tu, bali
dhambi zote. Usiogope kusema mbele za watu ya kwamba umeokoka, lakini pia
ninakushauri utafute kanisa lolote la kiroho ambalo utasikia Roho Mtakatifu
ndani yako akikuruhusu kwenda, na ujumuike nao katika ibada na uwaeleze ya
kwamba umeokoka na unahitaji msaada zaidi wa kiroho nao kwa jina la Yesu Kristo
wa nazareti aliye hai watakusaidia ili uishi maisha mazuri hapa duniani na
kisha utapata uzima wa milele
Lakini ngoja nikupe
siri hii, kwa kuwa umeokoka vita yako na shetani itakuwa kubwa sana. Sasa basi
hebu soma waefeso 6:10-20 kwa
kutafakari ili uzijue silaha ambazo zitakusaidia wewe kupambana na shetani. Na
ukizishika silaha hizo vizuri kwa msaada wa Roho Mtakatifu, ninakuhakikisia
ushindi kwako ni lazima.
Vitu vya Muhimu sana
kwako wewe uliyeokoka ni: neno(yoshua
1:8), ibada(yohana 4:23-24) na
maombi (wafilipi 4:6 na yohana 15:7)
NDUGU MPENDWA,
UBARIKIWE NA BWANA YESU. NINAKUPENDA!
MWISHO WA SOMO
By Clement
Emmanuel of Rij Company limited
No comments:
Post a Comment